Advertisement

Responsive Advertisement

MFANYABIASHARA MAARUFU ZANZIBAR AKAMATWA KWA TUHUMA ZA KUHUSIKA NA MATUKIO MAKUBWA YALIYOWAHI KUTOKEA ZANZIBAR

Jeshi la Polisi visiwani Zanzibar limemkamata mfanyabiashara Abdallah Ahmed Abdallah maarufu Machips (45), na fundi wa simu za mikononi, David Eliakim Odingo (32) kwa tuhuma za kuhusika na matukio makubwa yaliyowahi kutokea Zanzibar.
Naibu Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai Zanzibar, (DDCI), Salum Msangi alithibitisha kukamatwa kwa watu hao mnamo Septemba 19 mwaka huu akieleza kuwa wanaendelea kuhojiwa Tanzania Bara.
“Tumewakamata kutokana na tuhuma za kujihusisha na matukio makubwa yaliyotokea Zanzibar na watafikishwa katika vyombo vya sheria mara baada ya uchunguzi kukamilika,” alisema Msangi.
Alisema kwamba hali ya usalama kwa hivi sasa Zanzibar siyo mbaya lakini haipo salama kwa wahalifu kwa vile jeshi hilo linaendelea na operesheni yake ya kisayansi ya kuwatafuta na kuwakamata watu wote wanaojihusisha na vitendo vya uhalifu.
Hata hivyo, Msangi alisema kwamba Jeshi la Polisi linaendelea kuwatafuta wote watakaoguswa na matukio ya uhalifu yaliyotokea Zanzibar ikiwamo ya tindikali, milipuko na vitendo vya mauaji vilivyotokea katika miaka ya hivi karibuni.
Kukamatwa kwa watu hao kumefanya idadi ya Wazanzibari waliokamatwa na kufunguliwa mashtaka Tanzania Bara kufikia 24, baada ya kukamatwa kwa viongozi wa dini wakiwamo wa uamsho ambao wanakabiliwa na mashtaka ya kuhusika na vitendo vya ugaidi.
Habari za ndani zilizopatikana kutoka Jeshi la Polisi zinadai kuwa fundi David anayefanya shughuli zake maeneo ya Darajani, mfumo wake wa mawasiliano umebainika kuwa karibu na baadhi ya watu wanaoshikiliwa kwa tuhuma mbalimbali za matukio ya uhalifu yaliyotokea Zanzibar.
Kabla ya kukamatwa kwa Machips alikuwa alifanya shughuli zake za upigaji wa picha za mihadhara ya Kiislamu na harusi pia kuuza video zake katika duka lake liliopo katika eneo la Kwahaji Tumbo.
Tangu walipokamatwa hadi sasa watuhumiwa hao hawajafikishwa mahakamani kutokana na kuendelea kuhojiwa na Jeshi la Polisi kwa tuhuma mbalimbali zinazowakabili.
mwananchi

Post a Comment

0 Comments