Watu
zaidi ya 39 wamefariki dunia mjini Tehran nchini Iran baada ya ndege
waliokuwa wakisafiria kuanguka muda mchache baada ya kupaa kutoka katika
Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mehrabad.
Ndege ya abiria aina ya Antonov 140 iliyokuwa na watu 48 ilikuwa imepangiwa kuelekea katika mji wa Tabas, kaskazini mashariki mwa Iran.
Watu 9 wanaripotiwa kunusurika kifo katika ajali hiyo ya ndege huku hali ya baadhi yao ikiwa mbaya.
Afisa mwandamizi wa taasisi ya safari za ndege ameiambia PressTV kuwa, miongoni mwa abiria walikuwa ni watoto kadhaa.
Ripoti za awali zinaonyesha kuwa injini ya ndege hiyo ilifeli na kusababisha ajali hiyo.
Iran imewahi kukumbwa na ajali kadhaa za ndege na iliyokuwa mbaya zaidi katika miaka ya hivi karibuni ni ile ya mwaka 2011 ambapo ndege ya abiria ilianguka kaskazini magharibi mwa nchi na kusababisha vifo vya watu 77.
Julai mwaka 2009 ndege nyingine ya abiria ilianguka muda mfupi baada ya kupaa kutoka Tehran na kusababisha vifo vya abiria wote 168.
0 Comments