Advertisement

Responsive Advertisement

SHIRIKA LA SUMASESU MAKETE LAUNGA MKONO JITIHADA ZA KUBAINI VIVUTIO VIPYA VYA UTALII


Katika kuunga mkono jitihada za serikali kubaini aina mbalimbali za vivutio vya utalii mkoani Njombe, shirika lisilo la kiserikali la SUMASESU lililopo wilayani Makete mkoani hapo limeunga mkono jitihada hizo kwa kubaini mlima Ihobwela uliopo kata ya Tandala kuwa ni miongoni mwa vivutio vya utalii wilayani hapo

Aidha watumishi 16 wa shirika hilo wakiambatana na wageni 15 kutoka Ujerumani wamepanda mlima huo hivi karibuni na kubaini kuwa mlima huo unapaswa kuingizwa katika vivutio vipya vya utalii wilaya ya Makete kutokana na muundo wake pamoja na miti ya asili iliyopo katika mlima huo

Akizungumza na mwandishi wetu mara baada ya kupanda na kushuka salama katika mlima huo, Mkurugenzi wa shirika la SUMASESU Bw. Egnatio Mtawa amesema mlima huo una vilele vitatu tofauti vyenye mawe ya kuvutia pamoja na aina mbalimbali za mimea ya asili

Amesema ameamua kupanda mlima huo na watumishi wenzake pamoja na wageni waliowatembelea kutoka Ujerumani, ili kuona ni jinsi gani wilaya hiyo imejaa vivutio mbalimbali huku akisema kuwa ukiwa kwenye vilele vya mlima huo unaweza kuona vijiji mbalimbali vya wilaya ya Makete pamoja na Ziwa Nyasa
"Wilaya ya Makete ina vivutio vingi, mimi nitoe wito tu kwa jamii kuendelea kugundua na kuvibainisha vivutio mbalimbali vya utalii vilivyopo wilayani mwetu, ili serikali ivitambue na kuhakikisha vitaendelea kudumu na kuingiza kipato kwa wilaya na taifa kwa ujumla" amesema Mtawa
Amesema kuwa miongoni mwa wageni hao kutoka Ujerumani waliopanda mlima huo wapo walemavu wa aina mbalimbali ikiwemo ulemavu wa akili kwa viwango tofauti, lakini wameonesha ujasiri wa hali ya juu kwa kupanda mlima huo na kushuka wakiwa salama
"Mimi ni mara yangu ya kwanza kupanda mlima huu, mwanzoni nilikuwa nauona tu nikipita barabarani na kwa muonekano wake nilidhani ni vigumu ulivyo kaa mtu kuweza kupanda, na pia sikujua kama una vilele vitatu, mi nilijua kipo kilele kimoja tu, nawashauri wanamakete waje waupande huu mlima wajionee mandhari nzuri na uumbaji wa MUNGU ulivyo" amesema Mwaija Kisingile ambaye alifanikiwa kuupanda mlima huo

Mlima Ihobwela upo katika kata ya Tandala wilayani Makete na una vilele vitatu vyenye sifa tofauti tofauti na inapendekezwa na wadau hao serikali iangalie namna ya kuufanya kuwa vivutio vipya vya utalii na wananchi wanaouzunguka kuhakikisha wanatunza mazingira yake ili uendelee kuwepo
Na Edwin Moshi, Makete

Post a Comment

0 Comments