Advertisement

Responsive Advertisement

BUSARA YATAKIWA ITUMIKE BAINA YA POLISI NA CHADEMA


Na Ojuku Ibrahim MAAZIMIO ya Mkutano Mkuu wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) ya kuitisha maandamano na migomo isiyokoma nchi nzima kupinga kuendelea kwa vikao vya Bunge Maalum la Katiba (BMK) na baadaye kauli kali ya Jeshi la Polisi ya kukataza kitendo hicho na kutishia kutumia nguvu kuyazima, yanaweza kusababisha maafa kama busara hazitatumika kwa pande zote mbili.

Hayo yamesemwa na baadhi ya wananchi wa kada na vyama mbalimbali waliohojiwa kufuatia kuitwa polisi na kuhojiwa kwa Mwenyekiti wa Chadema Freeman Mbowe aliyetoa kauli hiyo wakati wa mkutano wa chama hicho hivi karibuni.

Chacha Maiya, aliyejitambulisha kama mwanafunzi wa sheria kutoka Chuo Kikuu Huria, alisema ingawa ni haki ya msingi kwa wananchi kuandamana, lakini tafsiri inayotokana na maneno ya Mbowe ni kama inayoashiria vurugu kutoka kwa wafuasi wake, jambo ambalo halikubaliki.

“Ni kama vile Mwenyekiti Mbowe anawahamasisha wafuasi wake kufanya vurugu. Nadhani kulikuwa na haja ya kuwa makini katika kutoa matamshi hasa unapotaka kuhamasisha umma, sasa suala la msingi ni kwa wao kusitisha maandamano yao na kufikiria njia nyingine ya kuwasilisha ujumbe wao kwa Rais au Bunge,” alisema.

Akizungumzia sakata hilo, kiongozi mmoja wa Chadema aliyeomba hifadhi ya jina lake, alisema kitendo cha polisi kuzuia maandamano yao hakiwezi kulipa uhalali Bunge Maalum kuendelea, isipokuwa wanazidi kuchochea ari ya wananchi katika kutafuta haki yao.

“Ipo siku watu watasema basi, imetosha, hivi vitisho vina mwisho wake, polisi wanataka kuingilia siasa kwa kuilinda CCM, lakini watambue kuwa hakuna sheria inayowapa mamlaka ya kuzuia maandamano ya kisiasa, walichopaswa kufanya, ni kutoa maelekezo ya namna ya kufanikisha maandamano hayo ili yatawaliwe na amani, siyo kupiga watu mabomu,” alisema.

Tokea kutolewa kwa maazimio hayo ya Chadema, wafuasi kadhaa wa chama hicho wamekamatwa katika maeneo mbalimbali nchini na wengine kufikishwa mahakamani, baada ya kujaribu kuandamana na polisi kutumia nguvu kuwazuia.

Post a Comment

0 Comments