RASIMU ya tatu ambayo imetolewa
hadharani juzi na Bunge Maalum la Katiba, imepokewa kwa maoni
mbalimbali. Baadhi ya wananchi wameipongeza kwa kuingiza mambo ya msingi
na wengine wameonesha kutoridhishwa na rasimu hiyo.
Wakizungumza na gazeti hili jana, baadhi
ya wasomi, viongozi wa dini na watendaji wengine wa taasisi mbalimbali,
walisema yapo mambo ambayo yamefuata kilio cha muda mrefu cha wananchi
wengi kama suala la mgombea binafsi.
Lakini, wengine wamesikitishwa na baadhi ya maoni ya wananchi kutupwa, kama la mawaziri kuteuliwa kutoka miongoni mwa wabunge.
Mgombea binafsi Mhadhiri Mwandamizi wa
Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dk Benson Bana alisifu rasimu kuwa na
mgombea binafsi na kuwa hicho ndicho kilio cha muda mrefu cha wananchi,
ambao wangependa kuwa na kiongozi asiyefungamana na upande wowote.
Alisema rasimu hiyo inatoa mwanya kwa
watu binafsi, waliokuwa wanatamani kuwania nafasi yoyote bila ya
kushiriki kupitia kwenye chama cha siasa.
“Sasa naamini watajitokeza wagombea
waliokuwa na kiu ya kuwania kupitia nyanja nyingine na sio siasa, hivyo
tunaweza kupata viongozi wasiotokana na vyama na tukafanya vizuri,”
alisema.
Kwa upande wake, Profesa Mkumbo Kitila
wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, alisema amefurahishwa na rasimu hiyo
kuzingatia mambo muhimu kama vile suala la mgombea binafsi na masuala ya
msingi kama vile ardhi.
Askofu Msaidizi wa Jimbo Katoliki la
Bukoba, Mhashamu Method Kilaini amezungumzia rasimu hiyo na kupongeza
baadhi ya vipengele, ikiwemo kuwepo kwa mgombea binafsi na Rais wa
Zanzibar kuwa Makamu wa Rais.
Makamu watatu wa Rais Katika eneo hili,
Dk Bana alisema wananchi wasiogope mfumo huo, kwani hakuna
kilichobadilika kwenye mfumo wa uongozi, bali ni majina tu yamebadilika
ili kukazia muungano.
Kwa upande wa Muundo wa Muungano, Dk
Bana alisema uamuzi uliofanywa wa kuacha muundo wa muungano, kupigiwa
kura ya maoni na wananchi wa pande zote, ni jambo zuri, ambalo ndilo
lililokuwa kilio cha watanzania wengi, ambao wanataka kuamua muundo wa
muungano.
Hata hivyo, alisema yapo mambo ambayo hayakuangaliwa kwa umakini, kama vile nafasi ya Tume ya Utumishi wa Umma.
Alisema katika hilo tume hiyo, haikupewa
nafasi kama jinsi tume nyingine mfano ya Mahakama na Bunge ilivyopewa
nafasi ya kupata watendaji wake na wajumbe wake na kwamba kwa tume ya
utumishi, ambayo ndiyo chombo kikuu cha watendaji wa umma,
haikuzingatiwa ipasavyo.
Alisema rasimu ya pili ya Warioba,
ilipendekeza kwenye Ibara ya 109, uwepo wa majina matatu
yatakayopendekezwa na tume kwenda kwa rais kwa ajili ya uteuzi wa nafasi
husika, lakini ibara hiyo imefutwa.
“Nimeshangaa kwa nini ibara hii
imefutwa, Tume ya Utumishi wa Umma ni kitu nyeti ambacho waombaji nafasi
za uongozi wa juu wangetuma maombi kwenye tume na tume kuchagua wenye
sifa na kisha majina matatu kupelekwa kwa rais kwa ajili ya uteuzi, ila
nashangaa kimefutwa”, alisema Dk Bana.
Alisema tume ya Mahakama na Bunge
zenyewe zimepewa nafasi hiyo na kwamba kufanya hivyo ni jambo muhimu,
ambalo linafanya kupatikana kwa viongozi wenye sifa, lakini jambo hilo
halikuzingatiwa kwenye tume hiyo ya umma ambayo ndiyo tume mama ya ajira
za watendaji serikalini.
Kwa upande wake, Profesa Kitila katika
masuala ya muungano na Makamu wa Rais, alisema Rasimu ya Bunge
imefunguka zaidi kwa upande wa Zanzibar, ambapo mambo ya msingi
yamezingatiwa, ikiwemo suala la muundo wa muungano, mambo ya muungano
kupunguzwa kuwa 14 badala ya 21. Profesa Kitila alisema suala la makamu
wa rais kuwa watatu, lina mkanganyiko kidogo hasa kwenye kipengele cha
mgombea mwenza.
“Ukitafakari kwa umakini utaona ni
kwamba suala la serikali tatu halikwepeki, ndiyo maana ya uwepo wa hizo
nafasi tatu za makamu wa rais, hicho kipengele cha mgombea mwenza hakina
mantiki”, alisema Profesa Kitila.
Hata hivyo, alisema Tume ya Jaji Joseph
Warioba ilipendekeza mabadiliko makubwa, kama yalivyokuwa kwenye rasimu
ya pili ya katiba mpya na kwamba rasimu hii ya tatu iliyowasilishwa na
bunge juzi, imekuja na maamuzi ya kawaida.
0 Comments